Saturday 31 December 2011

Mola Wako Anakuamrisha Uwafanyie Wema Wazazi Wako Ili Akulipe Pepo:

Anasema Allaah سبحانه وتعالى :

((وَقَضَى رَبُّكَ أَلاَّ تَعْبُدُواْ إِلاَّ إِيَّاهُ وَبِالْوَالِدَيْنِ إِحْسَانًا إِمَّا يَبْلُغَنَّ عِندَكَ الْكِبَرَ أَحَدُهُمَا أَوْ كِلاَهُمَا فَلاَ تَقُل لَّهُمَآ أُفٍّ وَلاَ تَنْهَرْهُمَا وَقُل لَّهُمَا قَوْلاً كَرِيمًا)) ((وَاخْفِضْ لَهُمَا جَنَاحَ الذُّلِّ مِنَ الرَّحْمَةِ وَقُل رَّبِّ ارْحَمْهُمَا كَمَا رَبَّيَانِي صَغِيرًا))


((Na Mola wako Ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote ila Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema. Mmoja wao akifikia uzee, naye yuko kwako, au wote wawili, basi usimwambie hata: Ah! Wala usiwakemee. Na sema nao kwa msemo wa heshima)) ((Na uwainamishie bawa la unyenyekevu kwa kuwaonea huruma. Na useme: Mola wangu, Warehemu kama walivyonilea utotoni)) [Al-Israa:23-24]

Ameanza Allaah سبحانه وتعالى katika Aayah hizo tukufu kutuamrisha tumuabudu Yeye Pekee bila ya kumshirikisha. Neno قَضَى 'Qadhwaa' ambalo kawaida lina maana kuwa ni 'Kakadiria' kutokana na makadario, hapa lina maana kwamba 'Ameamrisha'.

Kumuabudu Allaah سبحانه وتعالى kumeungamana na kuwaheshimu wazazi kwani Allaah سبحانه وتعالى Ameamrisha kuwafanyia wema baada ya kuamrisha kumuabudu Yeye kama Alivyounganisha vile vile katika aya nyingine ya kumshukuru kwanza Yeye kisha wazazi:


((وَوَصَّيْنَا الْإِنسَانَ بِوَالِدَيْهِ حَمَلَتْهُ أُمُّهُ وَهْنًا عَلَى وَهْنٍ وَفِصَالُهُ فِي عَامَيْنِ أَنِ اشْكُرْ لِي وَلِوَالِدَيْكَ إِلَيَّ الْمَصِيرُ))

((Na Tumemuusia mtu kwa wazazi wake wawili. Mama yake ameichukua mimba yake kwa udhaifu juu ya udhaifu, na kumwachisha ziwa baada ya miaka miwili. (Tumemuusia): Nishukuru Mimi na wazazi wako. Ni Kwangu Mimi ndiyo marudio)) [Luqmaan:14]

Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ametupa mafundisho katika Hadiyth zake nyingi kuhusu kuwaheshimu na kuwafanyia wema wazazi wetu:


عن أنس وغيره: أن رسول الله صلى الله عليه وسلم لما صعد المنبر قال: ((آمين آمين آمين)): فقالوا: يا رسول الله، علام أمنت؟ قال: ((أتاني جبريل فقال: يا محمد رغم أنف امرئ ذكرت عنده فلم يصل عليك، فقل: آمين. فقلت: آمين. ثم قال: رغم أنف امرئ دخل عليه شهر رمضان ثم خرج ولم يغفر له، قل: آمين. فقلت آمين. ثم قال: رغم أنف امرئ أدرك أبويه أو أحدهما فلم يدخلاه الجنة، قل: آمين. فقلت: آمين))


Kutoka kwa Anas na wengineo kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alipanda katika minbar na akasema:((Aamiyn, Aamiyn, Aamiyn)). Akaulizwa: Ewe Mjumbe wa Allaah, mbona umesema Aamiyn? Akasema: ((Amenijia Jibriyl na kuniambia: "Ewe Muhammad, amekhasirika yule anayekusikia (unatajwa) na hakuswalii". Akasema: "Sema Aamiyn", ndio nikasema Aamiyn. Kisha akasema: "Amekhasirika unayemfikia mwezi wa Ramadhaan na ukaondoka naye hakughufuriwa" (dhambi zake). Akasema: "Sema Aamiyn", ndio nikasema Aamiyn. Kisha akasema: "Amekhasirika yule anayekuwa mkubwa kisha wazazi wake wawili au mmoja wao bado yu hai, na wasiwe sababu yake kuingia Peponi". Akasema: "Sema Aamiyn", ndio nikasema Aamiyn)) [Tuhfat Al-Ahwadhiy 5:550]

Hadiyth nyingine:


عن أبي هريرة، رضي الله عنه، عن النبي صلى الله عليه وسلم قال: (( رغم أنف، ثم رغم أنف، ثم رغم أنف رجل أدرك والديه أحدهما أو كلاهما عند الكبر ولم يدخل الجنة))


Imetoka kwa Abu Hurayrah رضي الله عنه kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema: ((Amekhasirika, amekhasirika, amekhasirika, mtu ambaye wazazi wake wawili au mmoja wao wamefikia umri mkubwa (wa uzee) naye yu hai bado na haingii Peponi [kwa sababu ya kutowafanyia wema])) [Ahmad: 2:346]

Kuwafanyia wema wazazi kunaendelea hata kama mzazi mmoja au wote wawili wamefariki, wema huo unaweza kuuendeleza kwa kuwaombea Du'aa, kuwatolea sadaka, kuwafanyia Hajj na kadhalika, na yote yamethibiti katika Sunnah.

Kwa hiyo kama tunavyoona umuhimu wa kuwaheshimu wazazi wetu na kuwafanyia wema, basi tujitahidi kutekeleza amri za Mola wetu ili kupata Ridhaa Yake na Atulipe Pepo.

Sunday 25 December 2011

Mke Bora:

Mtungaji: 'Aliy 'Umar 'Uthmaan 1. Tupunguze mahari, mabanati waolewe Ili tuepuke shari, wenetu wasitiriwe Tuwatoe kwa fahari, tuombe wabarikiwe 2. Mke alivyoamriwa, dini yetu tuisome Kwake mefaradhiwa, sheria aziandame Lau mja husujudiwa, mke angeabudu mume 3. Akae nyumbani kwake, amlekee Mola pekewe Atimize wajibu wake, ibada kwa wakatiwe Jihadi ya mwanamke, ni kumtwii mumewe 4. Binti jikalie kwako, upate kusifika Mume ni rafiki yako, kumliwaza yataka Mume ni moshi wa koko, usipowaka hufuka 5. Husitiri siri yake, hampi labuda maiti Katu usiteteleke, usiwe yako hufiti Mtu hafui demu lake, katikati ya umati 6. Siku zote vumilia, mambo ngakusonga Nyumbayo shikilia, maisha vyema panga Mwana elewa dunia, ni pepo ya wajinga 7. Ufanye uvumilivu, uandame ule wakati Jikoni japo kukavu, ulimi wako dhibiti Asokujua alie wivu, aone una mno bahati 8. Waepuke wavundifu, tunga wako muamala Hali japo ni dhaifu, sitamauke kwa Mola Mtu haandami lufufu, ni matumizi na kula 9. Mja hujua atokako, dhiki nana usione Katu hujui wendako muatie Mola sinene Siri za nyumba yako, zisikeuke kuta nne 10. Hutopata utakacho, pepo tanga uandame Siwe nanga ubwiacho, ni hilo hilo siseme Shukuru upawacho, simkalifishe mume 11. Mwana soma upishi, hebu wata kukoroga Upike mule freshi, vyakula na maboga Basi hapo mutaishi, ya kweli sio soga 12. Uwe bora muandazi, uwalishe vya tiba Wape wanayo malezi, shirikiana na baba Waonyeshe mapenzi, japo riziki ni haba 13. Kupunguza gharama, na uipinge isirafu Huwa nusu ya kutuma, kujiwekea halafu Kuyafuja mali koma, kuna maji kuwa mafu 14. Pale mukiruzukiwa, ukumbuke na ukame Na dini tumeusiwa, muonee utungu mume Usipike visoliwa, mwana israfu ukome 15. Tunga mali ya mumeo, ni akibayo usivuju-usifujeni Siri ziweke pekeyo, sinene hata iweje Saza simalize leo, kesho shida zisije 16. Jilinde na machafu, umakinike uolewe Uepuke na uvundifu, wendapo usitahiwe Sifa ya mke ni upofu, asoona illa mumewe 17. Mke mwema ni kiziwi, haoni wala hasikii Asowasikiza wawi, raha mume kumtwii Na waovu hahadawi, uchafu hafikirii 18. Mke mwema ni kiduko, uzito kutiwa chuki Huviepuka vituko, hamtii mume dhiki Katu hana papatiko, mumewe hambanduki 19. Mke mwema huwa bubwi, asonena illa kheri Si umbile la lumbwi, kisema hutafakari Kinyume na chubwi, aolea juu ya bahari 20. Mke sawa awe kiwete, hakeuki kizingiti Katu hendi kokote, akikatzwa huketi Wa nidhamu saa zote, haupotezi wakati 21. Mwana siwe kirango, buibui kuwa ruhusa Katu sinene urongo, hilo ni kubwa kosa Lituze lako bongo, waume wawapi sasa? 22. Mwana guu silivute, bila ruhusa ya mume Kikatazwa usitete, shatani usiandame Radhi ya Mngu upate, katu nawe silalame 23. Utunge sana ulimi, siyanene yakaraha Hututongea ndimi, tukazikosa na raha Kama kweli umneni, basi nena ya furaha 24. Na mumeo mukiteta, sio mbele ya watoto Suluhu nawe tafuta, wala usione uzito Msamaha kishapata, ndio ulifumbe jito 25. Usimuinulie sauti, kimzungumzia mume Ikitokea tafauti, siropokwe jipime Alozalikana binti, ni mtele uso ndume 26. Saa zote jieke safi, japo ni kopo la maji Husifika mwanamke, upambe kiwa kipaji Mume hata atosheke, awe nde si mwendaji 27. Pale jito lifikapo, pawe swafi mwilini Kila nyote mukaapo, utumie lugha laini Hata kenda endapo, roho iwe nyumbani 28. Nguo japo tambara, uchachage lazima Bora upate sitara, dhikizo kutosema Usimame sana imara, usitikisike daima 29. Simnukishe uvundo, aingiapo nyumbani Ayaone kwa vitendo, ustaarabu wa pwani Umuoneshe na pendo, akiwa nde na ndani 30. Ujifukize na nyudi, jikwatue ndio ada Ujiweke maradadi, kwa viluwa na poda Mumeo roho iburudi, nakuusia ewe dada 31. Mama imekulazimu, una wajibu duniani Ulichozaa muhimu, yatie sana akilini Mama ndiwe mwalimu, wa wanayo nyumbani 32. Walee wanayo vyema, kwa misingi ya dini Waonee sana huruma, siwatese masikini Uhusiano uwe mwema, watakufaa mbeleni 33. Mpendee mume nduze, ulitunge na jinale Mume usimpeleleze, yuwatoa ngapi kule Muhimu atakeleze, katu haramu musile 34. Mtie mume urafiki, hata nde kusimueke Ili waja wanafiki, mabega yawashuke Ni wajibu yako haki, mtu kuzatiti chake 35. Marafikizo kwanda, watuje kwa makini Watague kama tunda, pale wendapo sokoni Uepuke asokupenda, kumjaza nyumbani 36. Watunge sana watu, usije matozi kulia Kuna wasojali kitu, na wenye mbaya nia Kitanda asisubutu, mwengineo kulalia 37. Linda faragha yako, wasione watu wote Uwe na mema mashiko, uyafuate kwa kite Mke chumbani kwako, mamnuu kwa yoyote 38. kama una uzuri- kama una uzuri bora, hutomshinda Hawa Wapili mrembo Sara, Ibrahimu alomkewa Vipusa walo na sura, na radhi za Moliwa 39. Mwana usiteteleke, usiwe nawe kama hao Jikaze mno umueke, mume ubora alonao Wele wao wanawake, wasotwii waume zao

Mashairi: Siku Macho Nikifumba (Sisitizo)

Twaha H. M Kiobya [Mujaahid] TIOT Morogoro 1. Bismillah naanza, kwa jina la utukufu Nia watu kuwafunza, Natumia hii safu Niepushe ya kuponza, wafanye uadilifu Hayatasaidia wafu, Masadaka ya matanga 2. Uloyatenda mwenyewe, kabla ya kutawafu Mazuri au yasiwe, atakulipa Raufu Hata kama usomewe, mahitaji maradufu Hayatasaidia wafu, ma-sadaka ya matanga 3. Wale nyama au sunga, hayafuti ulanifu Hawawezi pata mwanga, wale washibe wakinifu Haya ninyi mwajivunga, tatu hazifiki wafu Hayatasaidia wafu, ma-sadaka ya matanga 4. Ni uzushi kwenye dini, hajasema Ashrafu Si kitu arobaini, utapooza minofu Wale wakudanganyeni, ma vyakula na sarafu Hayatasaidia wafu, ma-sadaka ya matanga 5. Msimbe hayo yashike, mshairi maarufu Kwenye uzushi utoke, ufate wasadikifu Usingoje uumbuke, ya uzushi ni uchafu Hayatasaidia wafu, ma-sadaka ya matanga

Watu Aina Saba Watakaokuwa Katika Kivuli Cha Allaah (Subhaanahu Wa Ta'ala) Siku Ya Qiyaamah

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Kuna watu saba (7) ambao Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) atawafunika katika kivuli chake katika siku ambayo kutakuwa hakuna kivuli isipokuwa kivuli chake Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala)”: 1. Kiongozi Muadilifu; 2. Kijana aliyekulia katika kumcha Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala); 3. Muislamu ambaye moyo wake umesehelea katika msikiti; 4. Watu wawili wapendanao kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala), Kukutana kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) na kuachana kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala); 5. Mwanaume aliyeitwa na mwanamke mrembo kwa kutaka kufanya matendo ya haramu na akasema, “La hakika mimi namuogopa Allaah (Subhaanahu Wa Ta’ala)”. 6. Mtu anayetoa sadaka kwa mkono wa kulia na wa kushoto usijue kitu kilichotendeka (atoae sadaka kwa siri bila ya wengine kujua kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala), na 7. Mtu anayemkumbuka Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa faragha na huku macho yake yakatokwa na machozi.” (Al-Bukhaariy na Muslim) Katika Hadiyth hii nzuri Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kazungumzia kuhusu vitu vidogo vya ‘Ibaadah ambavyo ujira wake ni mkubwa mno: kivuli katika siku ambayo kutakuwa hakuna kivuli isipokuwa cha Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Hii inaweza kuonekana kuwa si jambo kubwa katika mara ya kwanza utakaposoma, lakini ukidhamiria katika Hadiyth ifuatayo; “Katika siku ambayo Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) atawafufua viumbe vyake vyote, jua litashushwa karibu sana na watu ambapo kutaachwa tofauti ya maili moja baina ya jua na watu ardhini. Watu watatopea katika jasho kulingana na amali zao, wengine mpaka kwenye vifundo vya vya miguu, wengine mpaka kwenye magoti yao, wengine mpaka kwenye viuno vyao na wengine watakuwa na hatamu ya jasho na, wakati yalivokuwa yanasemwa haya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliweka mkono mbele ya mdomo wake.” Imesimuliwa na Al-Miqdaad bin Aswad na imekusanywa katika Swahiyh Muslim - Juzuu ya nne (4), ukurasa wa 1487-8, nambari 6852. Na katika Hadiyth nyengine, watu wengine watatopea katika jasho “Sawa na urefu wa mikono sabini (70) katika dunia” (Al-Bukhaariy na Muslim) Nani atataka zaidi ya kuwa katika kivuli na hifadhi ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) katika siku hii. Wacha tu tuchunguze sasa sifa na fadhila za haya makundi saba (7) ya watu ambao wanastahiki na kuadhimikiwa na nafasi hii katika siku ambayo binaadamu wote watakusanyika. “Kiongozi Muadilifu…” Sheria/Haki katika Uislamu ni muhimu sana na ni kitu ambacho kila Muislamu Kiongozi na waongozwa lazima wafuate katika kila kitu bila ya hitilafu yoyote. Sheria ni kumpa kila mtu haki anayestahiki. Waislamu au wasio waislamu, ndugu au mgeni, rafiki au adui. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema: “Enyi mlio amini! Kuweni wasimamizi madhubuti kwa ajili ya Mwenyezi Mungu mkitoa ushahidi kwa haki. Wala kuchukiana na watu kusikupelekeeni kutofanya uadilifu. Fanyeni uadilifu. Hivyo ndio kuwa karibu mno na ucha Mungu. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu Anazo khabari za mnayoyatenda.” [Al-Maaidah: 8] Hata kama tunakubali katika kanuni, tunasahau haraka kwenye kufuata. Ndio maana unaona tukizungumza kuhusu marafiki zetu na watu walio karibu nasi, tunawasifia kupita kiasi, na tukizungumza kuhusu watu kinyume na hao, hatusemi hata jema moja lao na tunayakumbuka au kuyataja mabaya yao tu. Hii imetolewa na kutupwa kabisa katika sheria/haki ambayo Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anaipenda na hutoa ujira au thawabu kubwa mno kwaye, kama ilivotajwa katika Hadiyth ifuatayo: “Yule mtenda sheria atakuwa katika kiti cha enzi kwenye mkono wa kulia wa Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) – na hakika mikono yote ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) ipo kulia (haki) kwa wale ambao waadilifu wa sheria katika utawala wao, baina ya familia zao na kila kitu ambacho wamepewa mamlaka [Muslim]. Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimuagiza Abdullaah bin Mas’uud sehemu iliowazi katika mji wa Madiynah baina ya makazi na bustani ya mitende ya Answaar na aliposema Banu ‘Abd bin Zuhrah, “Watoe hapa kwetu watoto wa Umm ‘Abd (Ibn Mas’uud), akajibu, “Kwanini Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) amenileta mimi. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) hapendi wala hawarehemu watu baina yenu ambao hawatoi haki kwa watu walio dhaifu.” [At-Tirmidhiy] Kutekeleza Sheria kwa haki na uadilifu ni muhimu sana kwa mtawala yoyote, madhali yeye ndio mshika hatamu wa watu wake na yeye ndio mtoa haki wa mwisho katika sehemu husika, Kwa sababu hii, mtawala amepewa nafasi muhimu sana kama mmoja katika watu saba ambao watatunikiwa kivuli cha Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) siku ya Qiyaamah. “Kijana aliyekulia katika kumcha Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala)…” Mwanachuoni mkubwa Ayyuub as-Sakhtiyaaniy (aliyefariki mwaka 131H) amesema, “Kutokana na mafanikio anayokuwa nayo kijana, Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anamuongoza kuwa mwanachuoni wa Sunnah.” Hasan – Imesimuliwa katika Sharh Usuul as-Sunnah ya Imaam al-Laalikaa’iy (Namba 30). Kweli, ni baraka iliyoje kutoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa kijana ambaye ameongozwa kwenye ibada na akawa na urafiki au uongozo mzuri kwenye mambo mema, kwani kama tunavojua kuwa ni katika ujana wa mtu ambapo hukabiliwa na vishawishi vya dunia na huwa rahisi kuteleza kwenye njia ya Uislamu. Hii inakuwa dhihirifu pale tunapoana kwenye jamii zetu na tunaona hadaa nyingi za kidunia, kama muziki, michezo, vilabu mbali mbali visivo vya kheri, mambo ya fasheni na kadhalika. Hivi vyote huwa vimelenga au mlengwa mkuu katika mambo hayo tuliyoyataja hapo juu ni vijana. “Ujana huwa mara moja tu!” huwa wanaambiwa, na ndio maana Waislamu wengi siku hizi wanapoteza ujana wao kufikiri kuwa wataswali, watavaa Hijaab na kwenda kuhiji na kadhalika pale watakapofikia umri wa uzee, kama vile wana uhakikisho wa maisha marefu kutoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala)! Ewe ndugu yangu Muislamu ni kiasi gani tunajali wasia wa mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliposema: “Chukua faida ya mambo matano (5) kabla ya matano (5): ujana wako kabla ya uzee wako, afya yako kabla ya maradhi yako, mali yako kabla ya ufukara wako, faragha yako kabla ya wakati utakaoshughulishwa na mambo mbali mbali, na maisha yako kabla ya kifo chako.” [Al-Haakim] “Muislamu ambae moyo wake umesehelea (umeambatana) katika msikiti…” Kuna msisitizo mkubwa katika Sunnah kwa Muislamu mwanaume kuswali msikitini na malipo yake ni ni makubwa mno. Sio tu inamwezesha mtu astahiki kivuli cha Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) siku ya Qiyaamah, bali pia “…kila hatua anayochukua kuelekea msikitini hunyanyuliwa daraja moja na hufutiwa dhambi moja. Wakati akiswali, Malaika hawaachi kumuombea madhali yuko katika sehemu ya ibada na husema, Ewe Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma mrehemu mja wako huyu, Ewe Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma mhurumie mja wako huyu…” [Al-Bukhaariy] Hadiyth zote zinazowahamasisha wanaume kusehelea misikitini hazimaanishi wala hazikusudii kumuongoza mmoja kufikia timamu ya kwamba Uislamu ni Dini ambayo inatakiwa itekelezwe misikitini tu, kama watu wengi wanavofikiria. Misikiti inatakiwa iwe katika moyo wa jamii ya Kiislamu, na jukumu la wale wahusika wa msikiti ni kubwa na zito. Wao ndio wahusika wakuu wa kukaribisha stara kwa Waislamu, kuliko kuwa uwanja wa siasa na kitega uchumi kama ilivokuwa misikiti mingi siku hizi. Na tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Atuepushe na mambo kama haya kutokea! “Watu wawili wapendanao kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala), wakakutana kwa ajili ya Mola wao na wakatengana kwa ajili ya Mola wao…” Kuwa na upendo wa dhati kwa jili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) ni moja ya milango mitukufu kuelekea kwenye mazuri ya huko akhera na ni chanzo cha kuonja uzuri wa Imani katika dunia hii. Kupendana kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) inamaanisha Muislamu anatakiwa ampende Muislamu mwenzake kwa ajili ya usahihi au uongofu wa Dini yake. Bila ya kujali rangi, mtazamo wa kisura, anavaa nini, kama ni tajiri au maskini, anatoka wapi, au pengine ukachukia kila kitu chake ila ukampenda kwa ajili ya Imani yake: Huku ndiko kupendana kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). “Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema katika Hadiyth Al-Qudsiy: “Wale ambao wana upendo wa dhati kwa ajili ya Utukufu Wangu watakuwa na nguzo ya mwangaza, watahusudiwa na Mitume na mashahidi.” [At-Tirmidhiy na Musnad Ahman] SubhanAllaah! Fikiria kuhusudiwa na Mitume aliowachagua Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) mwenyewe, na wale waliofariki kwa ajili ya njia na radhi za Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala)!. Hayo ni malipo makubwa sana kwa wale wanaopendana kwa ajili ya Mola wao Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). “Mwanaume anayeitwa na mwanamke mrembo kwa kutaka kufanya matendo ya haramu na akasema “La hakika mimi namuogopa Allaah (Subhaanahu Wa Ta’ala)…” Dunia hii imejaa vishawishi ambavyo vinaelekeza kwenye moto wa jahannam na miongoni mwa hivyo vishawishi ni vile vinavotokana na wanawake. Wanaume wengi wameelekeza mioyo na nafsi zao kwenye maangamizi ya vishawishi vya wanawake na pia ndio maana Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akatuonya Ummah wake mahsusi kuhusu suala hili. Akasema, “Dunia ni nzuri na ya kijani na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Atakuwekeni na Atakufanyeni nyinyi kuwa mlioendelea ili Aone mutakayoyatenda. Basi Jiepusheni na ushawishi unaotokana na wanawake: Hakika mtihani wa mwanzo wa wana wa Israaiyl ulisababishwa na wanawake.” [Muslim] Ni muhimu sana kujiandaa na kujikinga kutokana na fitnah hii inayosababishwa na wanawake na vishawishi vengine vyote katika maisha kwa kumhofu Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Jambo hili hakika pia limezungumziwa katika Aayah ya Qur-aan ifuatayo: “Na ama yule anayeogopa kusimamishwa mbele ya Mola wake Mlezi, na akajizuilia nafsi yake na matamanio, Basi huyo, Pepo itakuwa ndiyo makaazi yake!.” [An- Naazi`aat: 40-41]. “Mtu anayetoa sadaka kwa mkono wa kulia na wa kushoto usijue kitu kilichotendeka (atoae sadaka kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa siri bila ya wengine kujua …” Hii inaeleza aina ya mtu anayeelekea katika umbali wa hali ya juu kabisa katika kujilinda na kujiepusha na Riyaa (kufanya amali njema ili watu wamuone na kumsifu). Dhambi hii kubwa inaangamiza faida ambazo zimo kwenye amali njema na husababisha adhabu kali kwa yule anayefanya jambo hilo. Ni hatari kwa kuwa ni tabia ya binaadamu kupenda na kufurahia watu wakimhimidi (wakimtukuza). Hivvo ni lazima tuwe makini sana na kuhakikisha kuwa nia zetu zinaanza na kuendelea kubakia kuwa safi kila mara tufanyapo amali njema kama kutoa sadaka. Sio kama tunavoona leo ambapo katika Misikiti yetu utakuta watu katika kipaza sauti na mabao ya matangazo yanayosema, ‘Fulani katoa kadhaa kumpa fulanikwa sababu kadhaa wa kadhaa! Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anaonya kwa kusema: “Enyi mlioamini! Msiharibu sadaka zenu kwa masimbulizi na maudhi, kama anayetoa mali yake kwa kuwaonyesha watu, wala hamuamini Mwenyezi Mungu wala Siku ya Mwisho. Basi mfano wake ni kama mfano wa jabali ambalo juu yake pana udongo, kisha likapigwa na mvua kubwa, ikaliacha tupu. Basi hawatakuwa na uweza wowote kwa walivyo chuma. Na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu makafiri…” [al-Baqarah: 264]. Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) atukinge katika jambo hili na atuongoze katika njia za kheri! “Mtu anayemkumbuka Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa faragha na huku macho yake yakatokwa na machozi.” Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametueleza: “Ingelikuwa unayajua ninayoyajua mimi, ungeli cheka kidogo na ukalia sana.” [Al-Bukhaariy] Kulia machozi sio alama ya udhaifu. Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ambaye alikuwa ndio binaadamu bora kabisa kuliko viumbe vyote, alikuwa akilia na pia Maswahaba zake wakifanya hivyo hivyo. Machozi ni njia thabiti ya kuonesha uoga wetu juu ya adhabu kali za Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala), upendo wetu wa dhati na kweli juu yake na hayaa (fazaa) juu yake. Lakini je, ni mara ngapi tunamkumbuka Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa faragha au upweke na huku machozi yakatutoka? Kiasi gani tunacheka na kufurahi kwa wingi na kulia kidogo sana? Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Hakuna kitu ambacho kinampendezesha na kupendwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kama matone mawili na alama mbili: Tone la chozi lilotoka kwa ajili ya kumwogopa Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala), na tone la damu lilitoka kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Na hizo alama mbili ni, alama iliyosababishwa kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala), na alama iliyosababishwa kwa kutimiza moja kati ya mambo ya fardhi yaliyoamrishwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala)…” [At-Tirmidhiy na katika Mishkaat] Alhamdulillaah, kwa mafunzo tunayoyapata kutokana na hawa watu wa aina saba (7) waliotajwa katika Hadiyth, tumepewa alama wazi wazi za kutuongoza katika kupata starehe na ridhaa au utoshelezi. Kwa hiyo, Ndugu zangu Waislamu tujitolee na tufanye jitihada kubwa ili tuwe miongoni mwa hawa watu saba, kwa hakika watu wenye bahati watakuwa wale watakaopewa kivuli cha Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) katika siku ambayo kutakuwa hakuna kivuli chochote isipokuwa cha Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) pekee. Aamiyn

Ndoa Na Sababu Za Kuchokana

akriban katika maisha ya wanandoa walio wengi kama sio wote, ndoa zao hupitia katika vipindi tofauti. Kama ulivyo umri wa Binadamu, ndoa hupitia katika kipindi cha utoto, ujana na uzee, na kila kipindi kina mambo yake na taratibu zake kama tulivyoona katika makala zilizopita ambazo kama wanandoa watashindwa kuzifuata basi huenda ndoa hiyo ikakumbwa na mtihani mkubwa, nao ni mtihani wa kuchokana. Hivyo basi, sababu kubwa ya wanandoa kuchokana, au kuzeeka kwa ndoa kunasababishwa na mwanamke, pale ambapo atashindwa kutumia nafasi yake na vipawa alivyopewa kuleta utulivu katika ndoa yao. Leo InshaAllaah tutahitimisha mfululizo wa makala haya kwa kugusia baadhi ya nukta ambazo ni muhimu kwa wanandoa kuzizingatia kabla na hata baada ya ndoa yao. DINI Kigezo Kikuu cha kusimamisha ndoa ni Dini, na ndoa yoyote inapokuwa haikuzingatia kigezo hiki basi ndoa hiyo inakuwa ina misukosuko isiyoisha, na si tu inapelekea wanandoa kuchokana, bali inapelekea wanandoa kutengana na kuchukiana. katika zama tulizonazo zama ambazo umagharibi umetawala katika mila na desturi zetu, kigezo cha Dini kimepuuzwa na familia nyingi za Kiislamu, na hata ainisho la neno ‘Dini’ limefahamika vibaya; Dini inaonekana ni imani ya kuzaliwa nayo, na si matendo na utaratibu wa maisha ya mtu. Na hii kupelekea mafunzo mengi ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kutofahamika katika usahihi wake, kwa mfano ile Hadiyth mashuhuri ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) iliyopokewa na Imaam Al-Bukhaariy inayohimiza kumchagua mchumba mwenye Dini: (...فاظفر بذات الدين تربت يداك...) (mchague mwenye dini utafanikiwa), mafundisho haya ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) yamekuwa yanatafsiriwa vibaya na wakati mwingine hata na Mashaykh, kuwa mwenye Dini ni yule Muislamu, hata kama haivai hijaab, haswali, fedhuli, lakini muda wa kuwa amezaliwa Muislamu basi huyo ana Dini, ufahamu huu umewaingiza wanandoa wengi katika mitihani. Bali wakati mwingine, unamkuta msichana amejihifadhi vizuri, anaswali lakini akhlaaq zake mbaya, msengenyaji, mfitinishi, hapendi ndugu wa mume, mchoyo na imani ya kweli haijagusa katika moyo wake, yeye huvaa Hijaab kama sehemu ya mila, na anaswali Swalah tano kutokakana na makuzi yake na mashinikizo ya kijamii, lakini hamna athari yoyote inayopatikana. Hivyo basi, ni muhimu kwa wanandoa wahakikishe kuwa ndoa yao inajengwa katika msingi mkuu na imara, msingi wa Dini kwa maana yake sahihi. HALI YA KIJAMII NA KIUCHUMI Katika ujenzi wa ndoa imara, kuna vigezo vingine ambavyo si muhimu lakini havipaswi kupuuzwa, miongoni mwa vigezo hivyo ni kiwango cha wanandoa kijamii na kiuchumi, hiki ni kigezo ambacho kinaweza kuonekana ni cha kidunia zaidi, lakini uzoefu unaonyesha kuwa kimekuwa ni moja miongoni mwa sababu zinazopelekea chokochoko katika familia na hatimae kuikwaza ndoa yenyewe. Inapotokea kwa mmoja miongoni mwa wanandoa hususan mwamume akawa na hali duni kiuchumi kuliko ile ya mkewe (familia ya mkewe) basi pamoja na mapenzi yanayowaunganisha, maisha yao yatakuwa na tahadhari kubwa sana, na wakati wowote kinaweza kutokea kitu ambacho hakikutarajiwa na kikazua mtafuruku. Hivyo basi, ni vema wanandoa wakaanza kujenga misingi imara ya ndoa yao kwa kujitahidi kuzingatia kigezo hiki cha Kiuchumi na Kijamii. KIWANGO CHA ELIMU Aidha ni muhimu kigezo hiki nacho kikazingatiwa katika ujenzi wa ndoa imara, kwani wanandoa kama tulivyoona katika makala zilizotangulia, wanahitaji kuwa na mazungumzo baina yao, mijadala tofauti tofauti na kubadilishana mawazo katika maisha, inapokuwa elimu ya mwanamke ni kubwa kuliko ya mwanamume, kwa mfano, mwanamke anapokuwa na shahada ya Chuo Kikuu, na mwanaume ya Darasa la Saba, hapa panahitaji hekima na juhudi kubwa kwa mwanamke kuweza kumuelimisha mumewe bila ya kumfanya ajihisi mjinga, zoezi ambalo ni gumu, na uwezekano wa kushindwa ni mkubwa. Mwandishi wa makala hii, ana ushahidi tosha wa ndoa zilizoharibika kutokana na kigezo hiki. Nawe msomaji unaweza kufanya utafiti wako binafsi kuhusu hoja hii. KABILA Uislamu unayazingatia makabila kuwa ni sehemu ya watu kufahamiana, na si vinginevyo, na umekaripia vikali ubaguzi wa aina zote zile ukiwemo ubaguzi kwa misingi ya ukabila, utaifa, na rangi, na katika hili kuna Aayah nyingi sana na Hadiyth nyingi za Mtume (Swalla Allaahu alayhi wa aalihi wa sallam). Kwa upande mwingine, jamii zetu za Kiislamu bado kwa kiwango kikubwa zinajenga mahusiano katika misingi ya ukaribu wa kikabila na uzoefu wa pamoja, Uislamu haujakataza mtu kujinasibisha na nasaba yake, kuipenda na kuitakia kheri, bali uislamu umekataza mtu kujifakharisha kwa ukabila na kudharau makabila mengine. Jamii za Kiislamu pamoja na kuunganishwa na Qur-aan na Sunnah za Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) lakini pia kila jamii inaunganishwa na vionjo vyake, na urfu zake ambazo huenda zikawa tofauti na jamii nyingine ya Kiislamu. Kwa mintarafu hiyo, ndoa inayowajumuisha watu wa kabila moja, inakuwa ina uimara zaidi kuliko ndoa tofauti, na inakuwa haina mashinikizo hasi kutoka katika jamii ukilinganisha na ile nyingine. NDUGU WA KARIBU Uislamu umeruhusu kwa baadhi ya ndugu wa karibu kuoana, mfano mtoto wa baba mkubwa kwa baba mdogo, mama mkubwa kwa mama mdogo, mjomba kwa shangazi, na ndoa hizi zimeenea sana katika baadhi ya jamii, na hata Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimuozesha binti yake Faatwimah (Radhiya Allaahu ‘anha) kwa mtoto wa ammy yake ambae ni 'Aliy Bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu), jambo la kushangaza ni kuwa baadhi ya Waislamu hususan huku Afrika wamejiharamishia ndoa za aina hiyo, bila ya dalili, jambo ambalo ni kwenda kinyume kabisa na mafundisho ya Kiislamu. Ndoa za ndugu wa karibu, zinaweza zikawa ni sababu ya kuimarika kwa ndoa au sababu ya kudhoofika, lakini kwa uzoefu wetu imeonekana kuwa ndoa za aina hii mara nyingi zinafikia katika hatua ya uzee mapema zaidi, hii ni kutokana na kufahamiana kwa ndugu hawa tangu utotoni, na kila mwanandoa kutotarajia jipya kutoka kwa mwenzake. HITIMISHO Ndoa ndio msingi wa Familia, na familia ndio tofali la kwanza la kujenga Jamii na hatimae kujenga Ummah, ndoa ni hatua muhimu sana anayopitia bianadamu katika maisha yake, na ndio hatua inayoiathiri maisha ya mtu na maisha ya kizazi chake baadae. Ni muhimu mtu kuwa makini sana na hatua hii. Kwa wale ambao tayari wameishaingia katika hatua hii, basi ni muhimu kwao kuizatiti ndoa yao na mafundisho sahihi ya Uislamu na kujaribu kurekebisha madhaifu yao kwa kuwa wawazi baina yao na kupeana mawaidha kwa njia ya upole na hekima. Maradhi ya kuchokana katika maisha ya ndoa ni maradhi yalioenea kwa wanandoa wengi, wapo wengine ambao hudhihirisha wazi hisia zao hizo kwa wenziwao, na wengine ambao huwa wanajaribu kuficha hisia hizo. Ni jukumu la kila mwanandoa kuelewa ukweli huo, na kujaribu mara kwa mara kuleta mabadiliko mema katika maisha yao, au kuikarabati ndoa kwa maana nyepesi.

Tofauti Baina Ya Mwanamume Na Mwanamke Katika Uislamu

Tabia na Maumbile: Mwanamme ameumbwa kutokana na udongo/tope/vumbi na mwanamke kaumbwa kwa ubavu. Allaah Amekadiria ada [hedhi] ya mwezi kwa mwanamke na sio kwa mwanamme. Mwanamme huota ndevu lakini mwanamke haoti, na ikiwa ataota basi anaruhusiwa kuzinyoa. Wanawake ni wapungufu wa ibada na uwezo wa kufikiri. Mathalan katika utoaji wa ushahidi, mwanamme mmoja ni sawa na wanawake wawili. Vile vile wakati wa ada zao za mwezi [hedhi] huwa hawafungi wala kuswali. Wanaume wamepewa madaraka juu ya kuwasimamia wanawake. Manii ya mwanamme ni meupe na ya mwanamke ni manjano. Ni wajib kufanyiwa tohara [jando] kwa mwanamme na ni Sunnah kwa mwanamke. Kutoga masikio kwa ajili ya mapambo kumeruhusiwa kwa wanawake na sio kwa wanaume. Twahara: Mkojo wa mwanamke una harufu kali na najsi zaidi kuliko wa mwanamme. Inapendekezeka kwa mwanamme kutia wudhuu tena pindi anapotaka kurejea pahali pale pale katika tendo la jimai. Swalaah: Adhana na Iqaamah sio lazima kwa wanawake na sio sawa kwa mwanamke kuadhini. Mwanamke huswali nyuma ya mwanamme, hata ikiwa mwanamke huyo yupo peke yake. Lakini mwanamme Swalaah yake itakuwa si sawa (haipendezi) ikiwa ataswali peke yake nyuma ya mwanamme mwenziwe. Mwanamke hawezi kuwa Imaam wa wanaume kwenye Swalaah. Ikiwa mwanamke anawaswalisha wanawake wengine, ni lazima asimame katikati ya safu. Wakati mwanamme aposwalisha husimama mbele peke yake. Swalaah ya Jama’ah ni waajib kwa wanaume na sio kwa wanawake. Safu iliyo bora kwa mwanamke katika Swalaah ya Jama’ah ni safu ya nyuma, na iliyo bora kwa mwanamme ni safu ya mwanzo. Imependekezwa kwenda kuswali Msikitini Swalaah za usiku kwa wanaume na sio kwa wanawake. Ikiwa Imaam atakosea katika Swalaah, mwanamke anatakiwa kupiga kofi lakini mwanamme hutakiwa kusema “Subhaana-Allaah” Wanawake hawalazimiki kuhudhuria Swalaah ya Ijumaa, wanaume ni lazima. Wanawake hawatoi khutbah ya ‘Iyd, Ijumaa, kupatwa kwa jua au mwezi, wala Swalaah ya kuomba mvua. Swalaah hukatika ikiwa mwanamke atapita mbele ya mwanamme anayeswali, na ikiwa mwanamme atapita mbele ya mwanamme anayeswali basi Swalaah yake huwa ni sahihi. Swalaah ya ‘Iyd ni waajib kwa wanaume, lakini si kwa wanawake. Hata hivyo imependekezwa kwa wanawake kuhudhuria ikiwa kutakuwa hakuna jambo litakaloleta fitna. Swalaah ya Maiti: Jama’ah husimama upande wa kichwani ikiwa wanamswalia maiti wa kiume na husimama katikati ikiwa ni maiti mwanamke. Haipendezi kwa wanawake kuzuru makaburini, lakini wanaume wameshauriwa kufanya hivyo. Wanawake hawawezi kusindikiza msafara wa mazishi, lakini wanaume wanaweza. Wanawake wanapokufa huoshana na kuvishana sanda wao kwa wao, na wanaume pia ni hivyo hivyo isipokuwa ikiwa ni mume na mke. Zakaah na Swadaqah: Wanawake wamehimizwa kutoa Swadaqah zaidi kuliko wanaume Mwanamke anaweza kuwapa Zakaah watoto wake na mumewe, lakini mwanamme hawezi kuwapa Zakaah watoto wake wala mkewe. Fidia ni jukumu lake mwanamme na sio mwanamke. Hii hutokea ikiwa mwanamme kwa makusudi kafanya kitendo cha ndoa na mkewe katika mchana wa mwezi wa Ramadhaan. Mwanamke hawezi kufunga Swawm za Sunnah bila ya ruhusa ya mumewe. Mwanamme anaweza kufunga Swawm za Sunnah bila ya ruhusa ya mkewe. Hijjah: Mwanamke ni lazima awe na mtu asiye weza kumuoa (Mahram) wakati wa safari. Mwanamke hatakiwi kunyanyua sauti yake wakati wa Talbiyah, mwanamme anatakiwa anyayue sauti yake. Ihraam ya mwanamke ni zile zile nguo zake za safari sio lazima nyeupe. Mwanamme anaweza kufanya Ramal, yaani kwenda mbio ndogo ndogo baina ya Swafaa na Marwaa, na kuizunguka Ka’bah; mwanamke hatakiwi kufanya hivyo. Haishauriwi kwa wanawake kujaribu kubusu au kugusa Jiwe Jeusi wakati wa msongamano. Mwanamme anaweza kupanda kilima cha Swafaa na Marwaa, mwanamke hatakiwi kufanya hivyo. ‘Aqiyqah Mtoto wa kiume huchinjiwa kondoo wawili, mtoto wa kike huchinjiwa kondoo mmoja. Jihaad, Vita, na Uongozi Hakuna wanawake waliokuwa Manabii wala Mitume. Mwanamke hawezi kuwa kiongozi wa watu wala jeshi. Mtume (Swalla-Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alifungamana agano kutoka kwa wanaume kwa kupewa mkono wa bay’ah na kaungwa mkono na wa wanawake kupitia matamshi. Si kama ilivyo kwa wanaume, Wanawake hawawajibiki kupigana Jihaad. Hata hivyo kuna baadhi ya hali ambazo ni lazima ziambatanishwe kabla wanaume hawajajiingiza katika wajibu huu. Ndoa, Talaka, na Eda: Wanawake wanapewa talaka, sio wanaume. Wanaume wana mamlaka ya talaka, ndoa na kutoa mahari; sio wanawake. Mwanamme anaweza kuoa mwanamke wa Ahlul-Kitaab [Mayahudi na Wakristo] ikiwa mwanamke huyo sio mzinifu. Mwanamke hana haki hii ya kuolewa na mwanamme wa Ahlul-kitaab. Mwanamme anaweza kuowa mke zaidi ya mmoja. Mwanamke hawezi kuwa na mume zaidi ya mmoja. Harusi na karamu ya harusi (walima) ni jukumu la mwanamme na sio mwanamke. Imeruhusiwa kwa wanawake kupiga dufu katika harusi zao. Hii hairuhusiwi kwa wanaume. Matengenezo, na majukumu na huduma za familia ni jukumu la wanaume na sio wanawake. Mwanamke yupo chini ya mamlaka ya mumewe. Mwanamme hayupo chini ya mamlaka ya mkewe. Mwanamke hawezi kutembelewa katika nyumba na mtu yoyote bila ya kupata ruhusa ya mumewe. Mwanamme hahitajii ruhusa kutoka kwa mkewe. Malaika humlaani mwanamke ikiwa atamtenga mume wake katika kitanda. Mwanamme hapati laana ikiwa atafanya hivyo. Mwanamke ni lazima apate ruhusa ya mumewe kabla hajatoka nyumbani. Mwanamme hahitajii ruhusa ya mkewe anapotoka nyumbani. Mwanamme hana eda isipokuwa anapotaka kumuoa dada au mama mdogo wa mke aliyemuacha. Hata hivyo ikiwa mwanamme atamuacha mkewe wa nne na akataka kumuoa tena basi itambidi amsubiri mpaka amalize eda yake. Mavazi na Mapambo: Mwanamke ameshauriwa kujipamba akiwa ndani ya nyumba yake na kwa ajili ya mume wake. Ni haramu kwa mwanamke kujishabihisha na wanaume kwa mavazi yao. Na mwanamume pia haipasi kujishabihisha na wanawake. Ni wajibu kwa wanawake kurefusha nguo zao zivuke chini ya vifundo vya miguu yao. Mwanamme kurefusha suruali na kanzu hadi zikavuka chini ya mafundo ya miguu ni haramu. Mwanamke hatakiwi abadilishe nguo zake isipokuwa akiwa yumo ndani ya nyumba yake au pahali pa stara. Haya hayapo kwa wanaume. Hijabu ya mwanamke ni lazima afunike mwili wote na uso. Wanawake wameruhusiwa kuvaa mapambo ila tu asiyadhihirishe kwa wasio mahaarim wake. Wanaume hawawezi kuvaa hariri, lakini wanawake wanaweza.

Aina Za Ndoa Na Hukumu Zake

Katika makala hii fupi inshaAllaah tutajaribu kuzitambulisha aina za ndoa na kuweza kuzijua hukumu zake kisheria pamoja na maelezo kwa ufupi. Ndoa ni mkataba unaofungwa na wanandoa kuhalalisha kila mmoja wao kuweza kustarehe na mwengine kwa mujibu wa sheria. Ndoa ni miongoni mwa alama na miujiza yake Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na ina dalili ya kuthibitika kwake katika Qur’aan na katika Sunnah. Katika Qur’aan Suuratu Nnisaa/3 وَإِنْ خِفْتُمْ أَلاَّ تُقْسِطُواْ فِي الْيَتَامَى فَانكِحُواْ مَا طَابَ لَكُم مِّنَ النِّسَاء مَثْنَى وَثُلاَثَ وَرُبَاعَ فَإِنْ خِفْتُمْ أَلاَّ تَعْدِلُواْ فَوَاحِدَةً أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُكُم “Na ikiwa mnaogopa kuwa hamtowafanyia mayatima uadilifu, basi oeni mnaowapenda katika wanawake, wawili au watatu au wanne. Na mkiogopa kuwa hamwezi kufanya uadilifu, basi mmoja tu, au wale ambao mikono yenu ya kulia imewamiliki.” Suuratu Nnuur/32 وَأَنكِحُوا الْأَيَامَى مِنكُمْ وَالصَّالِحِينَ مِنْ عِبَادِكُمْ وَإِمَائِكُم “Na waozeni wajane miongoni mwenu na wema katika watumwa wenu na wajakazi wenu.” Katika Sunnah يامعشر الشباب ، من استطاع منكم الباءة فليتزوج فإنه أغض للبصر وأحصن للفرج ، ومن لم يستطع فعليه بالصوم فإنه له وجاء أخرجه البخاري “Enyi vijana! Mwenye uwezo wa kuisimamia ndoa na aoe kwani huko ni kuweza kuinamisha macho na kuweza kuzikinga tupu na kama hamna uwezo basi ni juu yenu kufunga kwani huko ndiko kwenye kinga.” Al-Bukhaariy Na pia: النكاح من سنتي ، فمن لم يعمل بسنتي فليس مني Ndoa ni miongoni mwa Sunnah zangu na mwenye kutenda kinyume na Sunnah zangu hatokuwa pamoja na mimi. Ibn Maajah Ili ndoa ikamilike hupaswa kutimiza nguzo, masharti pamoja na adabu zake vinginevyo inaweza kuwa miongoni mwa ndoa zenye utata katika uhalali wake. Ndoa, kwa mujibu wa Rai za Jamhuur Ulamaa (isipokuwa Abu Haniyfah), zimegawika kwenye sehemu kuu tatu zifuatazo: 1 Ndoa sahihi iliyokamilika Iliyotimiza nguzo na masharti ya kusihi kwake na kuweza kutekelezwa. 2 Ndoa Sahihi isiyokamilika Iliyotimiza nguzo na masharti ya kusihi kwake lakini imeshindwa kutekelezwa. 3 Ndoa batili au fasidi Iliyokosekana moja ya nguzo au masharti ya kusihi kwake. Yanayopaswa kuwepo wakati wa kufungwa ndoa (Aqdi) Ni yafuatayo 1 Kuwepo mke na mume (ambao wataweza kuisimamia ndoa na kutokuwepo vizuizi vya kuwazuia kuoana)-miongoni mwa masharti ya ndoa. 2 Ijaabu (tamko la kuoa au kuozesha) na Qabuul (tamko la kukubali) - miongoni mwa nguzo za ndoa 3 Awepo walii -miongoni mwa masharti ya ndoa 4 Wawepo Mashahidi - miongoni mwa masharti ya ndoa Yanayopaswa kuzingatiwa Ni yafuatayo · Asiwe mmoja wa wanandoa ana vizuizi vya kuwafanya wasioane ikiwa ni vya muda au vya kudumu. · Mkataba wa ndoa uwe wa kudumu usiwekewe muda maalum. · Ridhaa, chaguo na uamuzi uwe ni wa wanandoa kusiwepo kulazimishana. · Wasiwe wanandoa katika hali ya kuhirimia kwa ajili ya Hajj au ’Umrah. · Yawepo mahari. · Wajulikane wanaooa au kuolewa. · Kusiwepo mbinu za kutoitangaza ndoa na kuificha. Ndoa batili au fasidi 1 NDOA FASIDI/ BATILI Iliyofisidika kwa kukosekana moja katika nguzo, masharti ya msingi ya kufungika ndoa. Ndoa hutakiwa ikamilike mambo yake yote zikiwemo nguzo masharti ya kusihi kwake ili iweze kuwa na uhalali kisheria. Haijuzu 2 NDOA WAKATI WA IHRAAMU Kuoa/kuolewa wakati mmeshahirimia ima kwa ibadah ya Hajj au ‘Umrah. Kuwepo katika hali ya Ihraamu ni moja katika mambo yanayomzuia mke/mume kufanya tendo la ndoa na kuoa au kuwakilishwa ndoa pia ni mambo yasiyofanywa kwa aliye kwenye Ihraamu. Haijuzu 3 NDOA BILA YA WALII Kufungwa ndoa kwa kuwepo mke na mume pamoja na mashahidi lakini Walii amekosekana. Ndoa haikamiliki bila ya kuwepo kwa Walii na ni mojawapo ya nguzo za ndoa. Walii ni mwenye haki ya kumuozesha na kusimamia ndoa kwa niaba ya binti. Haijuzu kwa mujibu wa Jamhuur Ulamaa na inajuzu kwa mwanamke aliye baleghe kujiozesha kwa mujibu wa rai ya Abu Haniyfah. 4 NDOA YA “WALII” ASIYEKUWA NA SIFA Kufungwa ndoa kwa kutimizwa masharti yote isipokuwa walii ni mama wa binti kwa kukosekana baba na mfano wake. Moja katika masharti ya kusihi ndoa ni kuwepo walii mwanamme. Kisheria walii ni mwanamme na mwanamke si miongoni mwa walii wa binti. Haijuzu 5 NDOA BILA YA KUWEPO MASHAHIDI Kufungwa ndoa wakiwepo mke na mume na walii bila ya kuwepo shahidi kama ilivyo ndoa ya Mut’ah au ndoa ya siri Ni moja katika masharti ya kusihi ndoa kwamba lazima ishuhudishwe na mashahidi ili kuondosha dhana ya kuwepo ndoa za siri na kuondosha tuhuma na dhana. Haijuzu Ndoa zenye utata katika kujuzu kwake NDOA MAELEZO SABABU HUKUMU 1 NDOA YA MUT’AH (MUDA MAALUM) Hufungwa kwa muda maalum japo masaa mawili, bila mashahidi wala walii, ambapo wanandoa kuwa na haki kama wameoana. Imewekewa muda maalum na hakuna kurithiana wala kutalikiana. Haijuzu 2 NDOA YA MHALILI (ALIYEACHIKA TALAKA TATU) Kuolewa mke aliyeachika talaka tatu si kwa lengo la ndoa bali kwa lengo la kuipinda sheria ili ahalalishiwe mume wa mwanzo. Mume anataka kurudiana na mkewe ambaye kamuacha talaka tatu na hivyo kumtafuta mume mwengine amuoe mkewe kwa makubaliano lakini pasipatikane tendo la ndoa kisha amuache. Kisheria atatakiwa aolewe na mume mwengine ndoa halisi na papatikane tendo la ndoa. Haijuzu 3 NDOA ZAIDI YA WAKE WANE Mume kuoa wake zaidi ya wane kwa wakati mmoja waliokubalika kisheria. Ruhusa na mipaka tuliyowekewa na sheria ni kuwa na wake wane tu kwa wakati mmoja. (Na hata kama mke ameachika talaka rejea na yupo katika eda basi uharamu upo pale pale). Haijuzu 4 KUOLEWA NA MUME ZAIDI YA MMOJA WAKATI MMOJA Mke kuolewa na mume zaidi ya mmoja kwa wakati mmoja yaani kuwa na waume wawili na kuendelea. Sheria inakataza mke kuolewa na waume wengi kwa wakati mmoja kwani ni kinyume na fitrah- maumbile ya asli (Uislamu). Haijuzu 5 NDOA KWENYE EDA Kumuoa au hata kumposa mke aliyeachika na bado yupo katika eda na hakuwa mke wake kabla. Kuwepo kwenye eda ya aina yoyote kwa mke ni kizuizi kinachomfunga kutoweza kuolewa mpaka imalizike isipokuwa kwa mtalaka wake tu kama mke aliyeachika talaka rejea. Haijuzu 6 NDOA KWENYE UJA UZITO KWA MWANAMKE AMBAYE HAJAPATA KUOLEWA KABLA Kwa mwanamke ambaye hajaolewa akazini na kupatikana ujauzito na kutaka kuolewa katika hali hii. Ndoa hizi hufanyika pale mambo yameshaharibika na kutaka kusitiriana Ujauzito utakuwa na hukumu sawa kama mwanamke aliye katika eda (Ahmad na Abu Haniyfah). Uja uzito hautokuwa na hukumu sawa kama mwanamke aliye katika eda (Maalik na ash-Shafi’iy). Haijuzu kwa rai ya Ahmad na Abu Haniyfah Inajuzu kwa rai ya Maalik na ash-Shafi’iy ila tu hatopaswa kustarehe naye mpaka ajifungue. 7 NDOA KWENYE UJA UZITO KWA ALIYEACHIKA Mke aliyeachika na ni mja mzito na kutaka kuolewa na mume mwengine asiyekuwa mtaliki wake. Mke aliyeachika katika uja uzito yupo katika Eda na humalizika atakapojifungua na kumaliza muda wake wa Nifasi. Kisheria Eda inamfunga mke kuolewa mpaka imalizike. Haijuzu 8 NDOA KWA ASIYEKUWA MUISLAMU WALA HAKUTEREMSHIWA KITABU Kuoa washirikina na makafiri ambao si miongoni mwa walioteremshiwa vitabu kama mayahudi na manasara. Moja katika masharti ya kusihi ndoa ni Uislamu. Hivyo kuoa asiyekuwa Muislamu huifanya ndoa kuwa fasidi. Haijuzu 9 NDOA KWA ASIYE MUISLAMU LAKINI NI MIONGONI MWA WALIOTEREMSHIWA KITABU Walioteremshiwa vitabu miongoni mwa mayahudi na manasara na wanaowafuata katika mila zao. Uislamu ni moja ya masharti ya kusihi ndoa ila kwa mujibu wa aya za Qur’aan wameruhusika kuolewa. Inajuzu ingawa ni Makruuh - haipendezi 10 KUOLEWA MUISLAMU NA ASIYEKUWA MUISLAMU Mwanamke wa Kiislamu kuolewa na kafiri, mwenye kumshirikisha Allaah pamoja na mayahudi na manasara. Ndoa hulazimisha utiifu wa mke kwa mumewe na hivyo kuwepo khofu ya kuweza kuathirika na kubadilisha dini na watoto kufuata dini ya baba. Haijuzu 11 KUOA/KUOLEWA NA ALIYERTADI Mwanamme au mwanamke aliyekuwa Muislamu kisha akaamua kurtadi – kutoka katika dini. Kwa kukosekana sharti la msingi la Uislamu na hata kama atakuwa amekwenda katika dini ya walioteremshiwa vitabu. Haijuzu 12 KUMUOA BINTI ULIYEZAA NJE YA NDOA Mwanamme kuoa binti aliyezaa baada kutembea (kuzini) na mama yake nje ya ndoa. Huyu ni mtoto wake kwani ni mbegu zake ila tu atakosa baadhi ya haki za kimsingi kwa kuzaliwa nje ya ndoa. Haijuzu 13 KUOA BINTI WA KAMBO AMBAYE MLIWAHI KUWA NA MAHUSIANO HARAMU NA MAMA YAKE Kuoa binti wa kambo ambaye mliwahi kuwa na uhusiano haramu (zinaa) na mama yake kabla. Si binti aliyezaa nje ya ndoa bali ni binti wa mama. Kutokana na kupatikana tendo la haramu la zinaa Maulamaa wametofautiana katika tendo hili (zinaa) je llitaweza kuharamisha halali (ndoa)? Na kuna Qaaidah-“Haramu haiwezi kuifanya halali nyengine kuwa haramu”. Kuna Qaaidah nyengine “tendo la haramu huharamisha halali”. Inajuzu kwa rai ya ash-Shaafi’iy na Maalik kwa sababu ya kutokuwepo dalili bayana kuharamisha. Haijuzu kwa rai ya Abu Haniyfah na Ahmad bin Hanbal kwa sababu ya kuwepo tendo la haramu zinaa. 14 KUOA BINTI WA KAMBO AMBAYE MLIWAHI KUWA NA MAHUSIANO HALALI NA MAMA YAKE Kuoa binti wa kambo ambaye kuliwahi kuwepo mahusiano ya halali (ndoa) na mama yake mzazi na binti huyu si miongoni mwa watoto wa mume. na Qaaidah – msingi wa kisheria yakipatikana maingiliano kwa mama huharamisha (kuolewa) binti yake. Haijuzu 15 KUOA MAMA AMBAYE ULIWAHI KUOA BINTI YAKE Kumuoa mama ambaye kabla mliwahi kuwa na uhusiano wa ndoa na binti yake. Haijuzu 16 NDOA KWA WALIONYONYA ZIWA MOJA Ikiwa watoto wa kike na wa kiume wametokezea kunyonya ziwa moja kwa mama mmoja na wakataka kuoana. Moja katika mambo yanayoharamisha ndoa ni kuoa /kuolewa na mliyenyonya ziwa moja kwani kitendo hiki tayari kisheria kimeshaunda udugu baina yao. Haijuzu 17 NDOA YA KUBADILISHANA (SHIGHAAR) Mwanamme kumuozesha binti/dada yake kwa mwanamme mwengine ambaye naye atamuozesha binti/dada yake kwa mwanamme wa mwanzo kwa mabadilishano. Ndoa hizi hufanyika pasi na kutajwa mahari kwani mahari ya kila mmoja ni kumkubalia mwengine kuoa kwake “nipe nikupe” na pasi na kupatikana ridhaa ya upande mwengine. Rai yenye nguvu haijuzu kwa kufanyika kinyume na misingi ya ndoa ya Kiislamu. 18 NDOA YA BOMANI Ndoa zinazofungishwa na wakuu wa wilaya au kwenye ofisi za wasajili wa ndoa serikalini. Hufanyika bila ya kutekelezwa masharti ya kimsingi katika sheria za ndoa za Kiislamu kwani si lazima kuwepo mashahidi au kuwa wanandoa ni wa dini moja. Haijuzu. Ikiwa taratibu za nchi zinahitaji kufungwa ndoa hii itawajibika kwanza kufungwa ndoa ya Kiislamu. 19 NDOA YA MISYAAR Mwanamke hukubali kuolewa huku akisamehe baadhi ya haki zake za kimsingi katika ndoa kama mahari, huduma na makaazi au hata katika kugawana siku (kwa wake wenza). Ndoa hizi hufanyika sana katika Bara Arabu hasa kutokana na ughali wa mahari na hivyo mke katika kutafuta stara huzisamehe baadhi ya haki zake. Na pia kama wenye kuoa Afrika huku wakiwa na mke mwengine na hivyo mke wa Afrika kusamehe baadhi ya haki zake kama za kugawana siku na nyenginezo kwa kuwa anapata huduma nyengine kama pesa na kadhalika. Itajuzu ikiwa imetimiza masharti ya kimsingi – Haitojuzu ikiwa haitotimiza masharti ya kimsingi kama kufanyika ndoa ya Misyaar bila ya Walii. 20 NDOA YA MISFAAR Hufungwa kwa muda maalum kama wakati wa mapumziko au kwa wafanyakazi, wanafunzi ambao wako mbali na miji au nchi zao humalizika baada ya kurudi sehemu zao walikotoka Kimsingi ndoa yoyote itakayowekewa mkataba/muda maalum kumalizika kwake haikubaliki kisheria kama ilivyo Mut’ah. Mfano wanandoa wamekubaliana kuoana wakiwa Uingereza tu lakini wakirudi walipotoka ndoa imemalizika hata bila ya talaka. Haijuzu kwa rai ya Jamhuur Licha ya kutimiza masharti yote ya kimsingi ila kwa kuwepo muwafaka wa kumalizika kwake ambao ni kinyume na taratibu za ndoa ya Kiislamu. Itajuzu kwa rai ya Abu Haniyfah ikiwa sharti la kumalizika halitozingatiwa kwani ni sharti batili. 21 KUOA MWANAMKE ALIYEPOSWA KABLA Kuvunja uchumba uliopo na kuposa kisha kumuoa binti ambaye tayari ameshachumbiwa. Kwenda kuposa mwanamke aliyeposwa ni haramu kisheria. Kwa mujibu wa Hadithi za Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam. Ikiwa atakayeposa anajua taarifa za kuposwa kwa binti kabla basi mtendaji ni mwenye madhambi na dhimma kwa kukiuka makatazo. Kama hakujua na kufahamu baadae basi uharamu upo pale pale Ndoa itajuzu kwa mujibu wa rai ya Jamhuur Ulamaa kwa sababu kilicho haramu kilitokea kabla ya kufungwa na si katika ndoa kwani khutba si miongoni mwa mwa masharti ya kusihi ndoa. Haijuzu kwa mujibu wa Maalik na kama ndoa itafanyika itabidi ibatilishwe 22 NDOA YA KUJIFICHA “SIRI” Kuoana kwa kukamilisha nguzo na masharti yote ya ndoa ila tu wanandoa na mashahidi kutakiwa kutoitangaza na kuidhihirsha. Ikiwa ndoa hii itakamilika katika idara zote ila kilichokosekana ni mashahidi tu kuitangaza ndoa. Kama kuoa mke wa zaidi ya mmoja bila ya kumtaarifu mke/wake/watu wengine. Inajuzu kwa sababu ndoa imekamilika kuwepo mashahidi kumeifanya si siri tena, imeshatangazwa. Ila ni jambo lisilopendeza kisheria (makruuh) 24 KUOA KWA NIA YA KUACHA Mume kuoa na katika mkataba wa ndoa akashurutisha kwamba atamuacha mke katika muda fulani au bila ya kushurutisha lakini tayari ameshaweka nia katika nafsi yake ya kuacha. Kimsingi ndoa yoyote itakayowekewa mkataba/muda maalum kumalizika kwake haikubaliki kisheria ikiwa imeshurutishwa au kuwekwa nia kwani inakuwa ndoa ya muda maalum. Na kuwepo ndani yake hadaa na udanganyifu. Haijuzu kwa rai ya Jamhuur kwa sababu ya kuwekewa muda wa kumalizika na udanganyifu. Itaweza kujuzu kwa rai ya Abu Haniyfah ikiwa shurti litabatilishwa na kutenguliwa Ni muhimu kwa kila Muislamu kuzifahamu vyema aina hizi na kuhakikisha ndoa yake imefungwa katika misingi na taratibu zilizo sahihi. Na kama ni miongoni mwa watakaosimamia au kuwakilisha katika ndoa wazingatie maelezo haya ili waweze kuwa na uelevu katika mwenendo mzima wa ndoa kuepuka matatizo na kuepukana na ndoa zenye utata. Pia kuwepo tayari kuusimamia ukweli na haki pale ambapo ndoa iliyofungwa ilifungwa katika misingi isiyokuwa sahihi au baadhi ya taratibu zake kukiukwa. Ikiwa ndoa ni moja katika alama zake Allah Subhaanahu Wata’ala na miujiza yake hatuna budi Waislamu kuhakikisha kuzithibitisha alama hizi kwa kuifunga katika misingi na taratibu sahihi za kisheria. Na Allah Ndiye Ajuaye zaidi

Umuhimu Wa Kutoa Zakaah Na Malengo Yake

Baada ya kumshukuru Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na kisha kumtakia rehma Mtume wake (Salla Allaahu ‘Alayhi Wasallam) tunawaletea somo la Zakaah kwa muhtasari hasa katika baadhi ya vipengele muhimu ambavyo vinatugusa katika jamii yetu. Somo hili limekuja baada ya kufanya utafiti mdogo tu katika mwaka 2004 hapa Uingereza kwa jamii ya Waislamu wanaozungumza Kiswahili ili kujua kama wanaitekeleza nguzo hii au vinginevyo. Mojawapo katika masuala yaliyokuwemo kwenye kidadisi ni kama mhusika ana elimu ya aina yoyote kuhusu Zakaah. Katika watu 75 waliojaza ni 26 tu waliokuwa wanaifahamu Zakaah na waliobaki hawakuwa na elimu ya kutosha kuhusu nguzo hii. Pia watu 65 walikubali kwamba wanaweza kuwa na sifa za kuweza kutoa Zakaah na ni 10 waliosema hawana sifa hizo. Na katika 65 waliokubali ni 25 waliosema kwamba wanaitekeleza nguzo hii kikamilifu. Katika sababu kadhaa zilizotajwa kwa Waislamu kushindwa kuitekeleza nguzo hii ni kuwa na imani dhaifu, uchoyo wa mali, kudhani kama kiwango kinachotolewa ni kikubwa, kuipenda dunia zaidi na kutozijua haki zake Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na pia upatikanaji wenyewe wa mali kutingwa na utata. Somo la Zakaah ni somo pana na lililosheheni elimu inayohitajika kwa kila mmoja wetu kulifahamu vyema ili aweze kuitekeleza nguzo hii kikamilifu kwani ni mojawapo katika nguzo tano za Kiislamu. Somo hili pia lilifanyika katika Darsa za Ramadhaan 1428, Septemba - Oktoba 2007 katika mji wa Northampton – Uingereza. Somo tumeligawa katika vifungu vifuatavyo kutokana na umuhimu wake na mazingira yaliyopo. 1. UMUHIMU WA KUTOA ZAKAAH NA MALENGO YAKE 2. MASHARTI YANAYOMUWAJIBIKIA MWENYE KUTOA ZAKAAH 3. ZAKAAH YA MAPAMBO YA DHAHABU 4. ZAKAAH YA FEDHA TASLIMU, BIDHAA NA MALI YA BIASHARA 5. KWA NINI MALI YA HARAMU HAITOLEWI ZAKAAH Tumeonelea tuzungumzie vipengele hivi kwani vina nafasi kubwa katika maisha yetu ya kila siku na pia kutokana na masuala mengi yanayoulizwa kuhusu Zakaah yameonekana kuelemea zaidi katika vipengele hivi tulivyoviainisha. Na pia ni kutoa picha na hima kwa wanaotaka kuitekeleza nguzo hii kuwa na sehemu ya kuweza angalau kupata msingi wa taratibu za nguzo hii muhimu. UTANGULIZI Moja katika mipangilio ni kwamba kila kitu kilichopo ni Chake Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na kumilikiwa na binadamu kama ni amana tu. Amana hii hukabidhiwa kwa muda tu na kwa masharti na jinsi Allaah (Subhaanahu Wata’ala) Anavyotaka. Na katika moja ya mipangilio yake (Subhaanahu Wata’ala) ni Zakaah. Neno Zakaah katika lugha ya kiarabu lina maana ya tohara, baraka, kutakasa na pia kuongeza. Kisheria ni kile kiwango cha mali ambacho Waislamu wanapaswa kukitoa ikiwa kama ni haki yake Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na kuwapa wanaostahiki. Ni nguzo ya tatu katika nguzo tano za Kiislamu na amri Yake Allaah (Subhaanahu Wata’ala) ambayo ni wajibu kutekelezwa na kila Muislamu mwenye uwezo. Zakaah si malipo, kodi, ada au takrima bali ni moja katika taasisi iliyoasisiwa na Allaah (Subhaanahu Wata’ala) ili kuleta uwiano katika neema Alizowajaalia waja wake. Zakaah ilifaradhishwa katika mwaka wa pili wa Kiislamu – Hijriyah kwa mujibu wa kauli yenye nguvu. Dalili za kufaradhiswa kwake ni aya zifuatazo katika Qur-aan: خُذْ مِنْ أَمْوَالِهِمْ صَدَقَةً تُطَهِّرُهُمْ وَتُزَكِّيهِم بِهَا Chukua sadaka katika mali zao, uwasafishe na uwatakase kwazo [At-Tawbah: 10] Vilevile: وَالَّذِينَ فِي أَمْوَالِهِمْ حَقٌّ مَّعْلُومٌ لِّلسَّائِلِ وَالْمَحْرُومِ Na ambao katika mali yao iko haki maalumu Kwa mwenye kuomba na anayejizuilia kuomba. [Al-Ma’arij 24-25] Na katika Sunnah: قال صلى اللّه عليه وسلم لمعاذ حين أرسله إلى اليمن‏:‏ ‏(‏أعْلِمْهُم أن اللّه افترض عليهم في أموالهم صدقة تؤخذ من أغنيائهم وترد على فقرائهم‏.‏‏)‏ أخرجه الجماعة‏.‏ Amesema Mtume (Salla Allaahu ‘Alayhi Wasallam) kumwambia Mu’aadh pale alipomtuma Yemen: “Wafundishe kwamba Allaah Amewafaradhishia katika mali zao sadaka (Zakaah) huchukuliwa kutoka matajiri miongoni mwao na kurudishwa kwa mafakiri” Imetolewa na Jamaa Zakaah na Sadaka ni maneno mawili ambayo humaanisha kitu kimoja kama ilivyokuwa katika Qur-aan na katika Sunnah za Mtume (Salla Allaahu ‘Alayhi Wasallam). Na pia wakati mwengine hutumika katika sura mbili ikiwa Zakaah ni Wajibu na sadaka ni isiyokuwa wajibu. UMUHIMU WA KUTOA ZAKAAH 1. Inawakumbusha Waislamu kwamba kila walichojaaliwa ni neema kutoka kwake (Subhaanahu Wata’ala) na Allaah Hupenda neema zake kutumika jinsi alivyoagiza. 2. Mwenye kutoa Zakaah hutekeleza ibadah na mojawapo katika nguzo kuu za Kiislamu. Ibadah ambayo kila Muislamu mwenye uwezo huwajibika nayo kuitekeleza. 3. Mwenye kupewa Zakaah hupewa ikiwa ni kama moja ya shukrani Zake Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na miongoni mwa haki zake. 4. Wenye kutoa Zakaah ndio waliojaaliwa sifa ya waumini wa kweli kwa mujibu wa Qur-aan إِنَّمَا يَعْمُرُ مَسَاجِدَ اللّهِ مَنْ آمَنَ بِاللّهِ وَالْيَوْمِ الآخِرِ وَأَقَامَ الصَّلاَةَ وَآتَى الزَّكَاةَ وَلَمْ يَخْشَ إِلاَّ اللّهَ فَعَسَى أُوْلَـئِكَ أَن يَكُونُواْ مِنَ الْمُهْتَدِينَ Wanaoamrisha misikiti ya Allaah ni wale wanaomuamini Allaah na siku ya mwisho na kusimamisha Sala na kutoa Zakaah na hawamuogopi yeyote isipokuwa Allaah basi hao ndio wanaotarajiwa kuwa miongoni mwa waliooongoka. [at-Tawbah: 18] ZAKAAH HUMSAIDIA MUISLAMU KATIKA MAISHA YA KIDUNIA Kwa: 1. Kupata radhi Zake Allaah (Subhaanahu Wata’ala). لَن تَنَالُواْ الْبِرَّ حَتَّى تُنفِقُواْ مِمَّا تُحِبُّونَ وَمَا تُنفِقُواْ مِن شَيْءٍ فَإِنَّ اللّهَ بِهِ عَلِيمٌ Hamtoweza kuufikia wema mpaka mtoe katika vile mnavyovipenda. Na chochote mtakachokitoa basi hakika Allaah anakijua. [Aali ‘Imraan: 92] 2. Kuzidisha baraka na kuongezeka kwa mali. وَمَا آتَيْتُم مِّن رِّبًا لِّيَرْبُوَ فِي أَمْوَالِ النَّاسِ فَلَا يَرْبُو عِندَ اللَّهِ وَمَا آتَيْتُم مِّن زَكَاةٍ تُرِيدُونَ وَجْهَ اللَّهِ فَأُوْلَئِكَ هُمُ الْمُضْعِفُونَ Na mnachokitoa kwa riba ili kiongezeke katika mali ya watu, basi hakiongezeki mbele ya Allaah. Lakini mnachokitoa kwa Zakaah kwa kutaka radhi ya Allaah, basi hao ndio watakaozidishiwa. [Ar-Ruum: 39] 3. Kuzidisha mapenzi na kuenziana katika jamii na kuzidisha udugu halisi wa Kiislamu وَالْمُؤْمِنُونَ وَالْمُؤْمِنَاتُ بَعْضُهُمْ أَوْلِيَاء بَعْضٍ يَأْمُرُونَ بِالْمَعْرُوفِ وَيَنْهَوْنَ عَنِ الْمُنكَرِ وَيُقِيمُونَ الصَّلاَةَ وَيُؤْتُونَ الزَّكَاةَ وَيُطِيعُونَ اللّهَ وَرَسُولَهُ أُوْلَـئِكَ سَيَرْحَمُهُمُ اللّهُ إِنَّ اللّهَ عَزِيزٌ حَكِيمٌ Na wanaoamini wanaume na wanaoamini wanawake ni marafiki wao kwa wao huyaamrisha yaliyo mema na huyakataza yaliyo mabaya na husimamisha Sala na hutoa Zakaah na humtii Allaah na Mtume wake. Hao ndio ambao Allaah Atawarehemu. Hakika Allaah ni Mwenye nguvu na Mwenye hekima. [At-Tawbah: 71] ZAKAAH HUMSAIDIA MUISLAMU KATIKA MAISHA YA AKHERA 1 Ni sababu ya kusamehewa madhambi yetu إِن تُقْرِضُوا اللَّهَ قَرْضًا حَسَنًا يُضَاعِفْهُ لَكُمْ وَيَغْفِرْ لَكُمْ وَاللَّهُ شَكُورٌ حَلِيمٌ Na mkimkatia Allaah sehemu nzuri (katika mali zenu mkazitoa kwa njia ya kheri) Atakuzidishieni na Atakughufurieni. Na Allaah Ndiye mwingi wa Shukrani na mpole. [At-Taghaabun-17] 2 Ni sababu ya kutakaswa na kusamehewa madhambi إِن تُبْدُواْ الصَّدَقَاتِ فَنِعِمَّا هِيَ وَإِن تُخْفُوهَا وَتُؤْتُوهَا الْفُقَرَاء فَهُوَ خَيْرٌ لُّكُمْ وَيُكَفِّرُ عَنكُم مِّن سَيِّئَاتِكُمْ وَاللّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ Kama mkitoa sadaka kwa dhahiri ni vizuri na kama mkitoa kwa siri na kuwapa mafakiri basi huo ni ubora zaidi kwenu na atakuondoleeni maovu yenu na Allaah Anazo habari za mnayoyatenda. [Al-Baqarah: 71] MALENGO YA KUFARADHISHWA KWAKE Zakaah imefaradhishwa na Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na ndani yake kuna malengo zaidi ya yale anayoyafahamu binadamu kwamba ni kwa ajili ya kuwasaidia maskini na wasiojiweza tu. Yafuatayo ni baadhi tu ya malengo yanayopatikana katika Zakaah kwa ufupi: 1 Humtoharisha Muislamu nafsi yake na kuondosha ubakhili katika mali kama ilivyoripotiwa kutoka kwa Shaykhul Islaam Ibnu Taymiyah (Allaah Amrehemu): نفس المتصدق تزكو، وماله يزكو، يطهر ويزيد في المعنى Nafsi ya mwenye kutoa Sadaka hutoharika na mali yake husafika na hutoharika na kuongezeka kimaana halisi. 2 Humuondoshea husda maskini na fakiri kwani ni khulka ya binadamu kuwa na choyo. 3 Huisafisha mali kwani haki iliyomo ndani yake haistahiki kubaki na mwenye mali si milki yake tena. 4 Huongeza baraka kwani kutoa Zakaah ni kutekeleza moja katika haki za mali. Ingawa mwenye kuitoa ataona kupungukiwa kwa mali kihali halisi lakini faida yake huwa ni baraka na neema. عن أبي هريرة رضي الله عنه أن النبي صلى الله عليه وسلم قال: ما نقصت صدقة من مال، وما زاد الله عبدًا بعفوٍ إلا عزًّا، وما تواضع أحد لله إلا رفعه الله رواه مسلم Kutoka kwa Abu Hurayrah Allaah (Amuwie radhi) amesema; Mtume (Salla Allaahu ‘Alayhi Wasallam) amesema: “Haitopungua mali kwa kutolewa sadaka na hamzidishii Allaah mja wake kwa kumnyima ila humfanya kuwa na nguvu na na yeyote mwenye kujidhalilisha kwa Allaah basi Allaah humnyanyua (daraja)” Muslim 5 Huondosha ufakiri katika jamii ikitekelezwa kikamilifu kwani tabaka la wasiojiweza hupungua na hatimae kutokomea. 6 Ni njia ya kujenga utamaduni wa kutoa kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu Wata’ala). Mwenye kuitekeleza nguzo hii humwia rahisi na kuwa na mazowea ya kutoa hasa katika amali nyengine za kheri. 7 Kuwapa mtihani waja wake kwani nafsi imeumbwa katika kupenda mali na utajiri hivyo kwa atakayekuwa tayari kutoa hufanya hivyo kwa ajili ya kutaka radhi Zake Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na hivyo kuvuka mtihani huu mzito. 8 Hujenga jamii yenye kusaidiana na kujaliana kwani uislamu unakataza kuwepo jamii inayoomba omba au isiyojitosheleza. Hili ni jambo la kuzingatiwa kwa kila anaeishi chini ya kivuli cha Kiislamu kuhakikisha mwenye uwezo kumsaidia asiyekuwa na uwezo. HEKIMA YA KUFARADHISHWA KWAKE Ni wajibu kuzingatia kwamba Allaah (Subhaanahu Wata’ala) hafaradhishi kitu isipokuwa kuna maslahi na faida. Tunaweza kuyaona maslahi yake na pia tusiyafahamu. Ila tu ni wajibu kwetu kuitakidi kwamba kila Allaah (Subhaanahu Wata’ala) Alichokileta basi kuna hekima ndani yake. Huu ni mmoja katika misingi ya Aqiydah sahihi ya Muislamu. Pia imethibitika kivitendo faida ya Zakaah ikitekelezwa kikamilifu enzi za Ukhalifa wa ‘Umar Ibnul ‘Abdil-‘Aziyz, (Allaah Amuwie radhi), ambapo iliweza kukusanywa na hakukuwepo maskini au mafakiri wa kupewa na iliishia Baytul Maal. Jamii iliweza kufikia hali ya maisha ambapo hakuna Waislamu waliokuwa wakihitaji Zakaah. Maulamaa wamezielezea hekima nyingi sana kama zifuatazo: 1 Kukamilika Uislamu wa mja Zakaah ni mojawapo ya nguzo za Kiislamu. Kuitekeleza ni kukamilisha mihimili mikuu ya dini yetu. Kila Muislamu ana wajibu wa kuzitekeleza nguzo zote 2 Alama ya ukweli wa kiimani Mali kimaumbile ni kipenzi na si rahisi mtu kukitoa anachokipenda isipokuwa apate kama kile au zaidi yake. Mwenye kutoa Zakaah hutaraji malipo zaidi na fadhila kutoka kwake Subhaana na huwa ni kitu kipenzi zaidi kwake. 3 Ni sababu ya kuingizwa peponi Kwa mujibu wa aya na hadithi nyingi zinazothibitisha hivyo. 4 Hufuta madhambi Zakaah humfutia madhambi mwenye kuitoa huku akikusudia kupata radhi Zake Allaah (Subhaanahu Wata’ala). ADHABU YA MWENYE KUACHA KUTOA ZAKAAH Katika mapendekezo yaliyotolewa kwenye kidadisi kuhusu Zakaah ilitajwa kuelezwa bayana athari na madhara yake kwa mwenye uwezo wa kuitoa Zakaah na hakufanya hivyo ikiwa ni kwa makusudi au kwa kutokusudia. Mwenye kuacha kutoa Zakaah kwa makusudi huku akijua kama ni wajibu kwake basi amekana moja katika nguzo za Kiislamu na hivyo kutoka katika dini – kurtadi. Pia ni moja katika madhambi makubwa ambayo adhabu kali imeandaliwa duniani na akhera kwa kila asiyetekeleza moja katika nguzo za Kiislamu ilhali anatambua umuhimu wake. Khalifa Abubakr Siddiyq (Allaah Amuwie radhi), aliandaa jeshi la Waislamu kwenda kupigana na Waislamu wenzi wao kwa sababu ya kuikataa nguzo hii. Na pale ‘Umar Ibnul Khattaab, (Allaah Amuwie radhi) alipomuhoji alimwambia: فإن الزكاة حق المال‏, ‏ والله لو منعوني عناقا كانوا يؤدونها إلى رسول الله صلى الله عليه وسلم لقاتلتهم على منعها‏ Hakika Zakaah ni haki ya mali na Wallaahi kama wakinizuilia hata kwa (kamba ya) kutiwa shemere (anayofungwa mnyama kwenye pua zake) nitapambana nao kwani walikuwa wakiitoa kwa Mtume (Salla Allaahu ‘Alayhi Wasallam). Adhabu zilizotajwa katika Qur-aan 1 Suurat At-Tawbah: وَالَّذِينَ يَكْنِزُونَ الذَّهَبَ وَالْفِضَّةَ وَلاَ يُنفِقُونَهَا فِي سَبِيلِ اللّهِ فَبَشِّرْهُم بِعَذَابٍ أَلِيمٍ يَوْمَ يُحْمَى عَلَيْهَا فِي نَارِ جَهَنَّمَ فَتُكْوَى بِهَا جِبَاهُهُمْ وَجُنوبُهُمْ وَظُهُورُهُمْ هَـذَا مَا كَنَزْتُمْ لأَنفُسِكُمْ فَذُوقُواْ مَا كُنتُمْ تَكْنِزُونَ Na wale wakusanyao dhahabu na fedha na wala hawazitoi kwa njia ya Allaah wape habari za adhabu inayoumiza (inayowangoja). Siku (mali yao) itakapotiwa moto katika Jahannam na kwa hayo vikachomwa vipaji vya nyuso zao na mbavu zao na migongo yao (na huku wanaambiwa) “haya ndiyo mali mliyojimbikizia (mliyojikusanyia) nafsi zenu basi onjeni (adhabu ya) yale mliyokuwa mkikusanya”. [Suurat At-Tawbah: 34-35] 2 Aali ‘Imraan: وَلاَ يَحْسَبَنَّ الَّذِينَ يَبْخَلُونَ بِمَا آتَاهُمُ اللّهُ مِن فَضْلِهِ هُوَ خَيْرًا لَّهُمْ بَلْ هُوَ شَرٌّ لَّهُمْ سَيُطَوَّقُونَ مَا بَخِلُواْ بِهِ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَلِلّهِ مِيرَاثُ السَّمَاوَاتِ وَالأَرْضِ وَاللّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ 3 Wala wasione wale ambao wanafanya ubakhili katika aliyowapa Allaah miongoni mwa fadhila zake kuwa ni bora kwao (kufanya ubakhili). Laa ni vibaya kwao watafungwa kongwa (minyororo inayofungwa kwenye shingo) za yale waliyoyafanyia ubakhili siku ya kiama Na urithi wa mbingu na ardhi ni wa Allaah. Allaah Anazo khabari za mnayoyafanya. [Aali ‘Imraan: 180] ADHABU ZILIZOTAJWA KATIKA SUNNAH وعن أبي هريرة رضي الله عنه قال‏:‏ قال رسول الله صلى الله عليه وسلم‏:‏ ‏(‏ما من صاحب ذهب ولا فضة لا يؤدي منها حقها إلا إذا كان يوم القيامة صُفِّحَت له صفائح من نار‏, ‏ فأُحْميَ عليها في نار جهنم‏, ‏ فيكوى بها جنبه وجبينه وظهره‏, ‏ كلما بردت أعيدت له في يوم كان مقداره خمسين ألف سنة حتى يُقْضَى بين العباد‏, ‏ فيرى سبيله إما إلى الجنة وإما إلى النار‏.‏‏)‏ رواه مسلم‏ Kutoka kwa Abu Hurayrah, (Allaah Amuwie radhi), Amesema Mjumbe wa Allaah (Salla Allaahu ‘Alayhi Wasallam) Mtu yeyote aliye na hazina na wala haitolei Zakaah basi atachomwa nayo katika moto wa Jahannam na itajaaliwa kama vinoo ambavyo atapigwa navyo kwenye migongo na vipaji mpaka Allaah Amalize kuhukumu waja wake siku ambayo ni sawa na miaka elfu khamsini. Kisha ndio ataoneshwa njia yake ikiwa kama ni ya peponi au motoni. [Muslim] Na amesema pia: "من آتاه الله مالاً فلم يؤد زكاته مثل له ماله يوم القيامة شجاعاً أقرع له زبيبتان يطوقه يوم القيامة، ثم يأخذ بلهزمتيه -يعني شدقيه- ثم يقول: أنا مالك أنا كنزك! ثم تلا: (وَلا يَحْسَبَنَّ الَّذِينَ يَبْخَلُونَ بِمَا آتَاهُمُ اللَّهُ مِنْ فَضْلِهِ هُوَ خَيْراً لَهُمْ بَلْ هُوَ شَرٌّ لَهُمْ سَيُطَوَّقُونَ مَا بَخِلُوا بِهِ يَوْمَ الْقِيَامَةِ) [آل عمران:180]" رواه البخاري. Mwenye kujaaliwa mali kisha hakuitolea Zakaah yake itageuzwa (mali hiyo) nyoka mwenye sumu kali ambae kichwa chake hakina manyoya na huku ana alama za vidoto viwili vyeusi kwenye macho yake. Nyoka atamzonga kwenye shingo yake na kumng’ata kwenye mashavu huku akisema: “Mimi ni utajiri wako mimi ndiyo hazina yako” Kisha akasoma: “Wala wasione wale ambao wanafanya ubakhili katika aliyowapa Allaah miongoni mwa fadhila zake kuwa ni bora kwao (kufanya ubakhili). Laa ni vibaya kwao watafungwa kongwa (minyororo inayofungwa kwenye shingo) za yale waliyoyafanyia ubakhili siku ya kiama” [Aali ‘Imraan: 180] al-Bukhaariy Na pia anasema Mtume (Salla Allaahu ‘Alayhi Wasallam) "ما منع قوم الزكاة إلا ابتلاهم الله بالسنين -المجاعة والقحط-" رواه الطبراني في الأوسط ورواته ثقات Hwatojizuia kaumu na kutoa Zakaah isipokuwa Allaah Atawapa mitihani ya ukame na njaa. At-Tabraaniy katika kitabu chake cha Al-Awsat na anasema wapokezi wake ni wenye kutegemewa. "ولم يمنعوا زكاة أموالهم إلا منعوا القطر من السماء، ولولا البهائم لم يمطروا" رواه ابن ماجه و البزار Na hawakujizuia kaumu na kutoa Zakaah ya mali zao isipokuwa Allaah Atawazuilia mvua kutoka mbinguni na lau kama si wanyama basi (mvua) isingelinyesha. Ibnu Maajah na Al-Bazzaar

Mbwa Wa Kufuga Je, Ni Najsi?

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu unajisi wa mbwa wa kufuga.

Mbwa mwenyewe hawezi kusemwa ni najisi kwa kutokuwa na dalili ya hilo, isipokuwa mate yake na majimaji ya puani mwake yanachukuliwa ni najisi kishari’ah ikiwa ni wa kufuga au vinginevyo kwa dalili iliyopatikana kutoka katika Hadiyth. Na kwa hivyo chombo chochote ambacho kitarambwa na mbwa kinapaswa kutwaharishwa kwa kuoshwa mara saba bila kutofautisha ni mbwa gani aliyekiramba, mojawapo kwa mchanga. Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Kukitwahirisha chombo kilichorambwa na mbwa kunafanywa kwa kuosha mara saba, mojawapo kwa udongo” (Ahmad, Muslim, Abu Daawuud na al-Bayhaqiy).

Na ikiwa ataramba chombo chenye chakula kikavu, kile chakula kilichoguswa na mdomo wa mbwa na kilicho pembezoni mwake kinatakiwa kitupwe, ama kilichobaki ni twahara kinaweza kubakishwa. Ama manyoya ya mbwa yakiwa makavu ni twahara. Sehemu iliyo najisi ya mbwa ni ule mdomo wake kwa ajili ya umandemande.

Hivyo, mtu kucheza na mbwa au kumpakata na kumfanya ni kichezeo, si jambo lenye kushauriwa kwa kupatikana uwezekano wa kunuswa au kurambwa nguo yake na maeneo ya kuswalia na sehemu mbalimbali za nyumba yake. Mbwa si kama paka, hivyo si jambo zuri watu kuiga tabia za wasio Waislamu na wao kuanza kufuga mbwa wa vichezeo na kuwafanya kama paka. Muislamu hata akibidi kuwa na mbwa wa ulinzi, anapaswa amweke nje ya nyumba; uani au sehemu ambayo si ndani ya nyumba ili kuepuka kutiliwa najisi vyombo, nguo na sehemu za kufanyia 'ibaadah.

Bonyeza viungo vifuatavyo upate maelezo zaidi:



Na Allaah Anajua zaidi